Alhamisi, 3 Septemba 2015

SOMO LA ASUBUHI LEO Alhamisi, Septemba 3, 2015

SHULE YA AKILI NA MAADILI 


Nao wauimba wimbo wa Musa, mtumwa wa Mungu, na wimbo wa Mwana-Kondoo, wakisema, Ni makuu, na ya ajabu, matendo yako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi; Ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa. (Ufunuo 15:3.)

Mwasisi Mkuu ameumba na kuzitengeneza mandhari mbalimbali katika maumbile [ulimwengu huu] ili zipate kuwa na maana kubwa katika tabia ya mwanadamu kiakili na kimaadili. Hizo zinatakiwa ziwe shule ya Mungu ya kuikuza akili na maadili. Hapo ndipo akili inaweza kuwa na nyanja pana sana ya utafiti katika maonyesho hayo ya matendo makuu ya Mungu wa milele. Miamba ni miongoni mwa vitu vya thamani ulimwenguni, ikiwa na hazina za hekima na maarifa. Katika miamba na milima hiyo umeandikwa ukweli kwamba hakika Mungu aliwaangamiza kwa Gharika wale waovu juu ya uso wa nchi hii. ----- MS 73, 1886.


Watu wale walijifikiria wenyewe kwamba walikuwa na hekima kuliko Mungu, na hekima ya kupindukia hata wasitake kutii... sheria na amri zake Yehova. Utajiri wa dunia hii aliowapa Mungu haukuwafanya kutii, bali kuasi, kwa sababu walivitumia vibaya vipawa vizuri vilivyotoka mbinguni, na kuifanya mibaraka ile waliyopewa na Mungu kuwa vitu vya kuwatenga mbali na Mungu. Na kwa kuwa walikuwa na tabia kama ile ya Shetani, badala ya ile ya Mungu, Bwana alituma maji ya Gharika juu ya ulimwengu ule wa zamani. ----- MS 62, 1886.

Mungu amejaa upendo, naye ni mwingi wa rehema; lakini kwa vyo vyote vile hataweza kuwaachilia [pasipo kuwapa adhabu] wale wasioujali wokovu wake mkuu aliowapa. Wakazi wale walioishi kwa miaka mingi sana kabla ya Gharika wakafagiliwa mbali kutoka juu ya uso wa nchi hii kwa sababu waliitangua sheria ya Mungu. Mungu hataleta tena maji kutoka katika mbingu za juu na chini ya nchi hii kama silaha zake za kutumia katika maangamizi ya ulimwengu huu; bali kisasi kinachokuja kitakapomwagwa juu ya wale wanaoyadharau mamlaka yake, [waovu] wataangamizwa kwa moto uliofichwa chini kabisa ya dunia hii, utakaochochewa sana na kufanya kazi yake kwa mioto ile itakayotoka mbinguni juu. Baada ya tukio hilo ndipo kutoka katika nchi hii iliyotakaswa utaimbwa wimbo huu wa sifa: "Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na yeye Mwana-Kondoo, hata milele na milele." Ufunuo 5:13. "Ni makuu, na ya ajabu, matendo yako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi; Ni za haki na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa [watakatifu]." Na kila mmoja aliyeifanya hazina ile ya mbinguni kuchukua nafasi ya kwanza katika mawazo yake, atajiunga kuimba wimbo huo mkuu wa ushindi.- RH, Feb. 24, 1885. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Toa maoni hapa...