Jumatano, 9 Septemba 2015

SOMO LA ASUBUHI LEO

YAKUPASA KUCHAGUA KUNDI LAKO


Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. 2 Wakorintho 6:17.

Mkristo wa kweli hatachagua kundi la wale ambao hawajaongoka. Iwapo Kristo ameumbika ndani, tumaini la utukufu, hatuwezi kufurahia hali ya hewa yenye malaria ya kiroho ambayo inazizunguka roho za wale wanaoipinga dini....

Marafiki zako wanaochukia kabisa mambo ya kiroho hawajatakaswa, hawajaadilishwa, wala hawajatukuzwa kwa kuiweka ile kweli katika vitendo. Hao hawako chini ya uongozi wake Kristo, bali chini ya bendera nyeusi ya mkuu yule wa giza. Kushirikiana na wale wasiomcha Mungu, wala kumpenda, isipokuwa kama unashirikiana nao kwa kusudi la kuwaongoa kwa Yesu, kutakuwa na matokeo mabaya kwa maisha yako ya kiroho. Kama huwezi kuwainua juu, basi, mvuto wao utaonekana juu yako kwa kuiharibu na kuitia waa imani yako. Ni vema kwako kuwatendea kwa upole; ila si vyema kwako kulipenda na kulichagua kundi lao, maana ukichagua hewa ile inayozizunguka roho zao, utapoteza urafiki wako na Yesu. Kwa njia zote zilizo katika uwezo wako jitahidi kuikomesha dhambi; walakini usiiruhusu dhambi hata kwa dakika moja kwa matendo yako, maneno yako, kimya chako, au kuwapo kwako. Kila wakati dhambi inaporuhusiwa na yule anayejidai kuwa ni mfuasi wake Kristo, utambuzi wake wa dhambi unadhoofika, na uamuzi wake kwa njia hiyo hupotolewa.... 

Bwana Yesu hawezi kumlinda mtu ye yote anayejiweka kwenye uwanja wa adui na kujizungushia marafiki wanaopendelea maongezi na tabia kama hiyo ambayo ni chukizo kwa Mungu anayemheshimu na kumpenda....

Ambatana kwa karibu sana na wale walio na mvuto unaoelekea kukuinua juu, ambao roho zao zimezungukwa na hali ya hewa iliyo safi na takatifu.... Mungu atakuwa karibu sana na moyo wako, zaidi hasa katika mawazo yako, kwa sababu umejitenga mbali na ulimwengu na mbali na mivuto ambayo ingekupeleka mbali na ile kweli, nawe hutaweza kuzingirwa sana na mitego ya Shetani. ----- Letter 51, 1894. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Toa maoni hapa...