Jumatatu, 20 Julai 2015

LESONI YA LEO JUMATATU Julai 20, 2015: Mmisionari wa Awali


"Ondoka, uende Ninawi!" lilikuwa ndilo agizo la Mungu kwa Yona. Katika Agano la Kale wito jwa kawaida ulikuwa "Njoni Sayuni." Mpango wa Mungu wa awali ulikuwa kwamba Isaeli wapate kuishi kivitendo kulingana na dini yao, kiasi cha kuwafanya Mataifa mengine wavutwe kuja kwao kutafuta ushauri (Isaya 56:70).

Yona kama mtangulizi wa wanafunzi katika Agano Jipya (Mathayo 28:18-20), anaagizwa aende Ninawi, mji ambao kwake ulionekana kuwa kitovu kichafu cha ibada ya sanamu, ukatili na ukandamizaji. Yona alifanya mikakati kuelekea magharibi kwa njia ya bahari japo Mungu alimwagiza kuelekea mashariki kwa nchi kavu. Yona, nabii mwenye kusita, alitoroka kuelekea upande tofauti na ule alioagizwa.

Somo Yona 1:3-17. Ni masomo gani tunayapata kutoka katika simulizi hii ya ajabu?

Jibu la mungu kwa utoro wa Yona lilikuwa katika sura ya dhoruba kubwa. Upepo humtii Muumba wake, japo nabii wake yeye hakutii (Marko 4:41). Yona alilala wakati wa dhoruba wakati mabaharia wapagani wanaomba (Yona 1:14). Kwa unyofu Yona alikiri kuwa yeye ndiye aliyesababisha dhoruba hiyo, na alitoa ushuhuda juu ya Mungu wa kweli na Mwumbaji. Zingatia kuwa jibu lake, "Mimi ni Mwebrania" lilitambulisha dini yake na taifa lake. Kwa kushtushwa na ukali wa ile dhoruba, wale mabaharia wapagani walijaribu kuokoa maisha yao na abiria, na kuonesha huruma kwa Yona wakasita kutii ushauri aliowapatia kuwa wamtupe baharini, dhoruba ilikwisha, na bahari ilitulia (aya ya 15). Mabaharia waliopigwa butwaa wakawa ndio waongofu wa kwanza wa Yona kwa Mungu wake, ambao walitenda kazi kupitia Yona hata pale alipokuwa anatoroka wito wake.

Wokovu wa Yona ulikuwa wa mwujiza kama ulivyokuwa wokovu wa meli. Mungu aliandaa "samaki mkubwa." Lugha ya asili ya Kiebrania haitaji ni aina gani ya samaki alimwokoa Yona kwa kummeza. Yona ndani ya tumbo la samaki ndio tukio mashuhuri sana katika kisa hiki; hata hivyo halipaswi kufunika ujumbe mkuu wa kitabu hiki kwamba Mungu anapenda, anajali, na anataka wokovu wa watu wote.

Mwisho, yupo Mungu mmoja tu, Muumba wa mbingu na nchi (angalia Isaya 44:8;45:5,6). Kingine chochote ambacho binadamu anakiabudu ni ibada ya sanamu na makosa. "Miungu" mingine yote wanayoiomba, ni ya kufikirika, na uongo mtupu. Kwa nini ukweli huu ni muhimu kwetu kuutambua na kuuzingatia kwa ajili yetu wenyewe, hasa katika muktadha wa utume?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Toa maoni hapa...